Waziri Mkuu, Dkt. Mwigulu Nchemba, Aprili 5, 2026, ameshiriki Tamasha la Pasaka la Mtoko na Christina Shusho lililofanyika katika Ukumbi wa Mlimani City jijini Dar es Salaam.
Akizungumza katika tamasha hilo, Waziri Mkuu amesema kuwa Pasaka ni kipindi muhimu kinachowakumbusha Watanzania kuishi kwa upendo, mshikamano na kudumisha amani katika jamii.
“Amani si kwa ajili ya faida ya Rais wala Serikali, bali ni kwa ajili ya kila mwananchi. Pasipo amani hata shughuli ndogo kama kujitafutia kipato haziwezi kufanyika.”
Ameeleza kuwa mnufaika wa kwanza wa amani ni mwananchi mwenyewe, kwani bila utulivu hata shughuli za kiuchumi, kijamii na ibada haziwezi kufanyika ipasavyo.

Aidha, amempongeza mwimbaji wa muziki wa Injili, Christina Shusho, kwa kuandaa tamasha hilo kubwa lililovuta maelfu ya waumini, akisema mafanikio yake yanaonesha kuwa lina kibali cha Mungu.
“Ukiona jambo linafanikiwa kiasi hiki, ujue lina kibali cha Mungu. Serikali haitakuwa kikwazo katika mipango ya kuendeleza huduma ya injili.”
Vilevile, Waziri Mkuu amewapa pole wafanyabiashara waliokumbwa na ajali ya moto ulioteketeza Soko la Mawasiliano (Simu 2000) lililopo katika Kata ya Sinza, Wilaya ya Ubungo, mkoani Dar es Salaam, iliyotokea Aprili 4, 2026, na kusema Serikali inafanya uchunguzi wa kina ili kubaini chanzo cha tukio hilo na kuchukua hatua stahiki.

Kwa upande wake, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mheshimiwa Patrobas Katambi, amesisitiza umuhimu wa wananchi kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama katika kudumisha amani na utulivu wa nchi.
“Ulinzi na usalama wa nchi ni jukumu la kila Mtanzania. Ni muhimu wananchi kuendelea kushirikiana na vyombo vya ulinzi na usalama ili kudumisha amani na utulivu wa nchi yetu.”
Tamasha hilo limehudhuriwa na viongozi mbalimbali wa Serikali, viongozi wa dini, pamoja na waumini na wadau wa muziki wa Injili kutoka ndani na nje ya nchi.

