ABDILATIF ABDALLAH-MGENI RASMI TUZO YA TAIFA YA MWALIMU NYERERE YA UANDISHI BUNIFU.

Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia Mhe.Prof.Adolf Mkenda amesema Hafla ya Nne ya Tuzo ya Taifa ya Mwalimu Nyerere ya Uandishi Bunifu Inatarajia kufanyika tarehe 13 Aprili 2026 jijini Dar es Salaam katika ukumbi wa Super Dome Masaki. 

Mhe. Adolf Mkenda ameyasema hayo April 8, 2026 jijini Dodoma, Wakati akizungumza na Waandishi wa Habari amesema, hafla hii hufanyika kila mwaka kuadhimisha siku ya kuzaliwa kwa Baba wa Taifa, Mwalimu Julius Nyerere na kutambua mchango wake katika kukuza lugha ya Kiswahili na utamaduni wa Taifa. 

Ameeleza kuwa Mwaka huu, mashindano yamehusisha nyanja nne za fasihi riwaya, hadithi za watoto, tamthiliya na ushairi.

 “Tunaendelea kukuza kiswahili, kuendeleza vipaji vya uandishi bunifu, kulinda historia na utamaduni wa Taifa, pamoja na kuongeza hifadhi ya vitabu katika maktaba ndio malengo ya tuzo hii”, amesema Prof. Mkenda.

 Sambamba na hayo Mhe. Adolf Mkenda amesema, Katika hafla hiyo mgeni rasmi anatarajiwa kuwa mshairi maarufu duniani Abdilatif Abdallah, mwenye asili ya Afrika Mashariki, ambaye aliwahi kufundisha Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kwa zaidi ya miaka 15. 

Hafla hiyo itatanguliwa na mjadala wa kitaaluma utakaoshirikisha waandishi bunifu wa Tanzania pamoja na wageni mashuhuri kutoka Uganda na Rwanda.