Wanaanga Waonekana Wenye Afya Njema Baada ya Kutua kwa Mafanikio

Wanaanga wa misheni ya NASA ya Artemis II wamefanikiwa kurejea duniani baada ya safari ya kihistoria ya kuzunguka mwezi, ambapo chombo chao cha anga, Orion, kilipita kwa kasi kubwa kupitia anga ya Dunia kabla ya kutua kwa mafanikio katika Bahari ya Pasifiki karibu na San Diego, California.

Chombo hicho kiliripotiwa kufikia kasi ya hadi maili 25,000 kwa saa wakati wa kurudi duniani, kikikabili joto kali lililokadiriwa kufikia nyuzi 3,000 Fahrenheit kabla ya mfumo wa parachuti kufanya kazi na kuhakikisha kutua salama.

Misheni hiyo ya siku 10 iliwahusisha wanaanga wanne: Reid Wiseman, Victor Glover, Christina Koch, na Jeremy Hansen wa Canada, ambao walizunguka mwezi na kufikia umbali wa mbali zaidi kuwahi kufikiwa na binadamu angani kuliko safari yoyote ya awali tangu enzi za Apollo.

Maafisa wa NASA wamethibitisha kuwa misheni hiyo imefanikiwa kwa asilimia kubwa, huku chombo hicho kikitua mahali palipopangwa bila matatizo makubwa.

Akizungumza baada ya tukio hilo, Msimamizi Mkuu wa NASA Jared Isaacman alisema misheni hiyo ilikuwa “kamili” na kuashiria mwanzo wa hatua mpya za Marekani kurudi kwa nguvu katika uchunguzi wa mwezi, ikiwa ni pamoja na mipango ya kujenga kituo cha kudumu cha mwezi ifikapo mwaka 2028.

“Tumerejea kwenye biashara ya kupeleka wanaanga mwezini. Huu ni mwanzo tu,” alisema Isaacman.

Baada ya kutolewa kwenye chombo chao na kupelekwa kwenye meli ya Jeshi la Majini la Marekani USS John P. Murtha, wanaanga hao walionekana wakiwa na afya njema na furaha, wakipunga mkono na kukumbatiana na maafisa wa NASA kabla ya kufanyiwa uchunguzi wa kitabibu.

Ripoti zinaeleza kuwa wanaanga wote waliweza kutembea wenyewe baada ya kurejea, ishara ya kupona vizuri baada ya athari za muda mrefu za hali ya uzito mdogo angani.

Misheni ya Artemis II sasa inatajwa kuwa moja ya hatua kubwa zaidi katika historia ya uchunguzi wa anga za juu, huku NASA ikianza maandalizi ya hatua zinazofuata za safari za mwezi na baadaye Mirihi