Rais wa Marekani, Donald Trump, amepunguza mvutano wa vita kwa kutangaza kusitishwa kwa mashambulizi dhidi ya Iran, huku mataifa hayo mawili yakikubaliana kusitisha mapigano kwa muda wa wiki mbili ili kutoa nafasi kwa mazungumzo ya amani.
Makubaliano hayo yanajumuisha kufunguliwa tena kwa njia muhimu ya kimataifa ya usafirishaji mafuta, Strait of Hormuz, ambayo imekuwa kitovu cha mvutano tangu vita ilipoanza mwishoni mwa Februari.
Kwa mujibu wa taarifa rasmi kutoka Tehran, Iran imekubali kushiriki mazungumzo na Marekani yatakayofanyika nchini Pakistan kuanzia Ijumaa, ikiwa ni juhudi za kumaliza mzozo huo uliotikisa uchumi na usalama wa kanda ya Mashariki ya Kati.
Waziri Mkuu wa Israel, Benjamin Netanyahu, amesema nchi yake inaunga mkono uamuzi wa kusitisha mashambulizi dhidi ya Iran, lakini akaweka wazi kuwa makubaliano hayo hayahusishi mapigano dhidi ya kundi la Hezbollah nchini Lebanon.
Hata hivyo, hali bado ni tete huku mashambulizi yakiendelea kuripotiwa katika maeneo mbalimbali ikiwemo Israel, Saudi Arabia na United Arab Emirates, jambo linaloonyesha kuwa utekelezaji wa makubaliano hayo bado una changamoto.
Taarifa pia zinaonyesha kuwepo kwa sintofahamu kuhusu vipengele vya makubaliano, hasa kuhusu mpango wa nyuklia wa Iran, baada ya kutolewa kwa matoleo tofauti ya makubaliano hayo kwa lugha ya Kifarsi na Kiingereza.
Wakati huo huo, Iran na Oman zinatarajiwa kutoza ada kwa meli zitakazopita katika mlango wa Hormuz, hatua inayoweza kuwa na athari kubwa kwa biashara ya kimataifa ya mafuta.
Tangu kuanza kwa vita hiyo, maelfu ya watu wamepoteza maisha huku miundombinu muhimu ikiharibiwa, hali iliyoongeza shinikizo kwa pande zote kutafuta suluhisho la kudumu.
Licha ya makubaliano hayo ya muda, wachambuzi wanaona hatua hiyo kama dirisha la kidiplomasia lenye matumaini, lakini wakionya kuwa mvutano uliopo bado unaweza kulipuka upya iwapo makubaliano hayatatekelezwa kikamilifu.