Azam yafikisha sare kumi Ligi Kuu Bara

AZAM imeendelea kuangusha pointi katika Ligi Kuu Bara msimu huu kupitia matokeo ya sare baada ya kumaliza dakika 90 zingine bila kufungana ugenini dhidi ya Mbeya City.

Matokeo ya mechi hiyo iliyochezwa leo Alhamisi Aprili 9, 2026 kwenye Uwanja wa Tanzanite Kwaraa jijini Babati mkoani Mantara, yanaifanya Azam kufikisha pointi 34, ikisalia nafasi ya tatu, chini ya Simba yenye 36 na vinara Yanga (44).

Sare hiyo ni ya pili mfululizo kwa Azam ambapo wikiendi iliyopita ilitangulia kupata matokeo kama hayo ilipokuwa nyumbani dhidi ya Simba.

Azam sare hiyo isiyo na mabao inakuwa ya saba kati ya kumi ilizopata msimu huu lakini ikiendelea kutamba na rekodi yake ya kutopoteza msimu huu kama ilivyo kwa Yanga. Azam ndiyo timu yenye sare nyingi kwenye Ligi Kuu Bara msimu huu ambazo ni kumi, ikishuka dimbani mara 18, ikishinda nane.

Licha ya sare hiyo, Azam itajilaumu yenyewe kushindwa kupata ushindi kwenye mchezo huo, baada ya kupoteza nafasi nyingi za kufunga kupitia kiungo wake Feisal Salum aliyepoteza nafasi tatu za wazi na Jephte Kitambala.

Mbeya City licha ya kuwa mwenyeji lakini haikufanya mashambulizi makali kwa Azam ambapo nafasi moja pekee ambayo watajilaumu ni dakika ya 78, kipa wa wageni Aishi Manula alipodaka vizuri mpira wa kichwa uliokuwa unaingia wavuni ukipigwa na mshambuliaji Vitalis Mayanga.

Kwa Mbeya City, matokeo hayo yanazidi kuishusha na presha ya kushuka daraja licha ya kwamba haipo salama sana kufuatia kusalia nafasi ya 12 na alama 17.

Azam ambayo iliifunga Mbeya City mabao 2-0 kwenye mchezo wa duru la kwanza, inakuwa imevuna jumla ya alama nne mbele ya wagonga nyundo hao wa Mbeya.