Jeshi la Marekani limetangaza kuwa litaweka kizuizi baharini dhidi ya usafiri wote wa majini unaoingia na kutoka katika bandari na maeneo ya pwani ya Iran kuanzia leo Jumatatu, Aprili 13, 2026.
Hatua hiyo inakuja baada ya mazungumzo ya mwishoni mwa wiki kushindwa kufikia makubaliano ya kumaliza vita kati ya Marekani na Iran, hali inayotishia kusambaratisha usitishaji wa vita wa muda wa wiki mbili.
Mazungumzo hayo yaliyofanyika Islamabad, Pakistan, yalianza Jumamosi iliyopita hadi alfajiri ya Jumapili, na yalikuwa ya kwanza ya moja kwa moja kati ya Marekani na Iran kwa zaidi ya muongo mmoja.
Pia, yalikuwa mazungumzo ya ngazi ya juu zaidi tangu mapinduzi ya Iran ya mwaka 1979, yaliyobadili kabisa mfumo wa uongozi wa Iran.
Majadiliano hayo yalifanyika siku chache baada ya kusitishwa kwa mapigano yaliyokuwa yameanza Jumanne, yakilenga kumaliza vita vya wiki sita vilivyosababisha vifo vya maelfu ya watu katika ukanda wa Ghuba, kuathiri vibaya usambazaji wa nishati na kuzua hofu ya vita kubwa zaidi katika eneo hilo.
Kamandi Kuu ya Jeshi la Marekani (CENTCOM) imesema kuwa kizuizi hicho kitaanza saa 10:00 alfajiri kwa saa za Marekani Mashariki na kitatekelezwa bila ubaguzi dhidi ya meli za mataifa yote zinazoingia au kutoka katika bandari za Iran, ikiwemo bandari zote zilizoko katika Ghuba ya Uajemi na Ghuba ya Oman.
Hata hivyo, jeshi hilo limeeleza kuwa meli zinazopita katika Mlango Bahari wa Hormuz kuelekea au kutoka bandari zisizo za Iran hazitazuiwa. Taarifa zaidi zitatolewa kwa mabaharia wa kibiashara kupitia matangazo rasmi kabla ya kuanza kwa operesheni hiyo.
Rais wa Marekani, Donald Trump, amesema jana Jumapili kuwa vikosi vya nchi hiyo pia vitaanza kukamata meli yoyote katika maji ya kimataifa ambayo italipa ushuru kwa Iran.
“Hakuna mtu atakayelipa ushuru haramu na bado apite salama katika bahari za kimataifa,” ameandika Trump katika mitandao ya kijamii. Ameongeza kwa msisitizo: “Muirani yeyote atakayefyatua risasi kwetu au kwenye meli za amani, atalipuliwa vibaya!”
Aidha, amesema Jeshi la Wanamaji la Marekani litaanza kuondoa mabomu ya baharini yaliyodaiwa kuwekwa na Iran katika Mlango Bahari wa Hormuz, ambao ni njia muhimu inayopitisha takribani asilimia 20 ya mafuta yote yanayosafirishwa duniani.
Taarifa za usafirishaji wa majini zimeonesha kuwa meli tatu kubwa za mafuta zilivuka mlango huo Jumamosi, lakini hadi kufikia Jumatatu, meli nyingi zilikuwa zikiepuka njia hiyo kwa hofu ya kuanza kwa kizuizi cha Marekani.
Kutokana na hali hiyo, bei ya mafuta ghafi katika soko la kimataifa ilipanda kwa zaidi ya asilimia saba na kufikia zaidi ya dola 100 kwa pipa katika biashara za asubuhi barani Asia. Wakati huohuo, Dola ya Marekani imepanda thamani, huku hatima ya soko la hisa la Marekani ikionesha kushuka.
Dana Stroul, aliyewahi kuwa ofisa mwandamizi wa Wizara ya Ulinzi ya Marekani wakati wa utawala wa Joe Biden, amesema hatua hiyo ni ngumu kutekeleza kwa muda mrefu.
“Trump anataka suluhisho la haraka, lakini ukweli ni kwamba operesheni kama hii ni ngumu kuitekeleza peke yake na haiwezi kudumu kwa muda wa kati au mrefu,” amesema Stroul, ambaye sasa anafanya kazi katika taasisi ya Washington Institute for Near East Policy.
Kwa upande wa Iran, Jeshi la Walinzi wa Mapinduzi ya Kiislamu limeonya kuwa meli za kijeshi zitakazokaribia Mlango Bahari wa Hormuz zitachukuliwa kuwa zinavunja makubaliano ya kusitisha mapigano na zitachukuliwa hatua kali.
Ofisa mmoja wa Marekani amesema Iran ilikataa matakwa ya Marekani ya kusitisha kabisa urutubishaji wa madini ya uranium, kuvunja mitambo yote mikubwa ya urutubishaji na kuhamisha nje akiba yake ya uranium iliyorutubishwa kwa kiwango cha juu.
Pia, Iran ilikataa shinikizo la Marekani la kusitisha ufadhili kwa makundi kama Hamas, Hezbollah na Wahouthi, pamoja na kufungua kikamilifu Mlango wa Hormuz.
Vyombo vya habari vya Iran vimeripoti kuwa kulikuwa na makubaliano katika baadhi ya masuala, lakini mgogoro mkubwa ulihusu mlango huo wa kimkakati pamoja na mpango wa nyuklia wa Iran.
Waziri wa Mambo ya Nje wa Iran, Abbas Araghchi, amesema nchi yake ilikumbana na masharti magumu, kubadilishwa kwa makubaliano na hatua ya kizuizi wakati mazungumzo yalipokuwa karibu kufikia makubaliano ya Islamabad.
“Hakuna funzo lolote lililopatikana. Nia njema huzaa matokeo mazuri, na uadui huzaa uadui,” amesema.
Hata kama usitishaji vita utaendelea kudumu, wachambuzi wanaamini kuwa itachukua muda kwa usambazaji wa nishati kurejea katika hali ya kawaida katika ukanda wa Ghuba. Hali hiyo inatarajiwa kusababisha kupanda kwa bei za mafuta na kuongeza mfumuko wa bei duniani.
Rais Trump amekiri kuwa bei ya mafuta na petroli huenda ikaendelea kuwa juu hadi uchaguzi wa katikati ya muhula utakaofanyika Novemba, kauli inayotafsiriwa kama kukubali athari za kisiasa zinazoweza kusababishwa na vita hiyo.
Kwa upande wake, Spika wa Bunge la Iran, Mohammad Bagher Qalibaf, amechapisha ramani ya bei za mafuta katika eneo la Washington akisema: “Furahieni bei za sasa. Kwa kizuizi hicho cha Marekani, hivi karibuni mtakumbuka enzi za petroli ya dola 4 hadi 5.”
Kuhusu mustakabali wa mazungumzo, Trump amesema anaamini Iran itaendelea kushiriki katika mazungumzo, akiyaita yale ya Islamabad kuwa ya kirafiki.
“Hakuna mtu mwenye akili timamu anayeweza kusema anataka silaha za nyuklia bila kuwa na karata yoyote mkononi,” amesema.
Hata hivyo, baadaye alibadilisha msimamo wake akisema hana shida ikiwa Iran haitarejea kwenye meza ya mazungumzo.
“Ikiwa hawatarudi, sina shida,” amesema Trump baada ya kurejea Washington kutoka Florida.
Kwa upande mwingine, Qalibaf ameilaumu Marekani kwa kushindwa kujenga imani na Iran licha ya kile alichosema kuwa ni mapendekezo ya mbele yaliyotolewa na Tehran.
Rais wa Iran, Masoud Pezeshkian, katika mazungumzo yake na Rais wa Russia, Vladimir Putin, amesema Iran bado inataka makubaliano ya haki na yenye usawa.
“Ikiwa Marekani itarejea katika misingi ya sheria za kimataifa, kufikia makubaliano si jambo gumu,” amenukuliwa akisema.
Kwa ujumla, hali inaendelea kuwa tete katika eneo la Ghuba, huku kizuizi cha Marekani kikiongeza hatari ya mvutano mkubwa zaidi. Hatua hiyo inaweza kuwa na athari kubwa si tu kwa usalama wa eneo hilo, bali pia kwa uchumi wa dunia, hasa katika sekta ya nishati inayotegemea sana njia ya Mlango Bahari wa Hormuz.
