Ushirikiano mpya wa elimu kati ya Tanzania na Chuo Kikuu cha Limerick cha Ireland unaibuka kama nguzo muhimu ya kimkakati katika kufanikisha Dira ya Taifa ya Maendeleo ya 2050.
Hatua hiyo inalenga kuweka rasilimali watu, sayansi na teknolojia katika kitovu cha mageuzi ya uchumi wa nchi.
Mkataba uliosainiwa hivi karibuni katika Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kati ya Wizara ya Elimu, Sayansi na Teknolojia na taasisi hiyo ya Ireland, unapanua programu ya ufadhili wa masomo iliyokuwapo na kuigeuza kuwa mfumo mpana wa ushirikiano wa serikali kwa serikali, unaolenga ujuzi, utafiti na ubunifu.
Kiini cha makubaliano hayo ni Programu ya Ufadhili ya Samia (Samia Extended Scholarship Programme – DS/AI+), inayolenga kuwajengea vijana wa Kitanzania uwezo katika sayansi ya data, Akili Unde (AI) na nyanja zinazohusiana, ujuzi unaotajwa kuwa muhimu katika uchumi wa dunia wa baadaye.
Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia, Profesa Adolf Mkenda, alisema makubaliano hayo yanaashiria dhamira ya Tanzania kuelekea uchumi unaotegemea maarifa.
“Ushirikiano huu umekuja wakati mwafaka, wakati Tanzania ikiendelea kuwekeza katika kujenga uchumi unaotegemea maarifa na ubunifu,” alisema.
Moja ya vipengele muhimu vya makubaliano hayo ni uamuzi wa Chuo Kikuu cha Limerick kugharamia asilimia 50 ya ada kwa wanafunzi wa Kitanzani; hatua inayopunguza mzigo kwa Serikali na kupanua fursa za kupata elimu bora ya kimataifa.
Kwa sasa, wanafunzi 32 wanasoma Ireland chini ya programu hiyo, huku wengine 16 wakiwa Afrika Kusini, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuwapatia wanafunzi uzoefu wa mifumo ya elimu ya kimataifa.
Wanafunzi hao walichaguliwa mwaka 2025 na kuandaliwa kupitia mafunzo ya miezi 10 katika Taasisi ya Sayansi na Teknolojia ya Nelson Mandela (NM-AIST).
Kwa watunga sera, kundi hili si wanufaika wa ufadhili pekee, bali ni msingi wa nguvu kazi ya baadaye itakayochochea viwanda, mageuzi ya kidijitali na ubunifu chini ya Dira ya 2050.
Balozi wa Ireland nchini Tanzania,? Nicola Brennan, alisisitiza nafasi ya elimu katika mafanikio ya nchi yake, akitoa mfano unaoweza kuigwa na Tanzania.
“Elimu ni muhimu sana kwa Ireland. Ni moja ya sababu zilizotuwezesha kufikia ukuaji wa uchumi, ustawi na maendeleo,” alisema.
Alibainisha kuwa uwekezaji endelevu katika elimu tangu miaka ya 1960 uliiwezesha Ireland kujenga nguvu kazi yenye ujuzi wa hali ya juu, hali iliyovutia kampuni za kimataifa na uwekezaji wa moja kwa moja kutoka nje.
“Kama taifa dogo, tumefanikiwa kuvutia kampuni za kimataifa kwa sababu tuna nguvu kazi yenye ujuzi mkubwa,” alisema.
Kauli hiyo inakuja wakati muhimu kwa Tanzania, ambayo inatarajiwa kuwa na idadi ya watu zaidi ya milioni 120 ifikapo mwaka 2050, hali inayoongeza umuhimu wa ajira na uzalishaji.
“Msingi wa kuhakikisha vijana wanapata ajira na kuunda fursa uko kwenye elimu,” alisema Brennan, akihimiza uwekezaji endelevu katika elimu bora.
Mbali na ufadhili wa masomo, makubaliano hayo yanaweka msingi wa ushirikiano wa muda mrefu katika utafiti, kubadilishana utaalumu na kuimarisha uwezo wa taasisi kama mambo muhimu katika kujenga mfumo imara wa ubunifu.
Mjumbe wa kamati ya ushauri ya programu hiyo, Dk Aikande Kwayu, alisema mpango huo unaendana moja kwa moja na malengo ya maendeleo ya Tanzania.
“Huu ndio ujuzi utakaotawala siku zijazo. Kwa kuwekeza kwa vijana sasa, Tanzania inajenga utaalamu unaohitajika kushindana kimataifa,” alisema.
Aliongeza kuwa uzoefu wa kimataifa utawasaidia wanafunzi kupata si tu maarifa ya kitaaluma, bali pia uwezo wa kufikiri kwa kina na kutatua matatizo.
Kwa Tanzania, mtihani mkubwa utakuwa jinsi ya kuwaunganisha wahitimu hawa katika uchumi ili kuleta mabadiliko iwe katika viwanda, utafiti au ujasiriamali.
Profesa Mkenda alisema Serikali inatarajia ushirikiano huo kupanua fursa, kuimarisha utafiti na kuleta matokeo ya maendeleo yanayoonekana.
Wakati kundi la kwanza la wanafunzi likiendelea na masomo yao, ushirikiano huu wa elimu kati ya Tanzania na Ireland unaonekana si tu kama mpango wa ufadhili wa masomo, bali uwekezaji wa muda mrefu katika rasilimali watu, uwekezaji unaoweza kuamua mwelekeo wa nchi kuelekea uchumi wa ujuzi na ubunifu ifikapo mwaka 2050.