SERIKALI YATANGAZA VIPAUMBELE VYA MAENDELEO YA VIJANA 2026/2027

Na Janeth Raphael MichuziTv -Dodoma 

Waziri katika Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Joel Nanauka, amesema kuwa katika mwaka wa fedha 2026/2027, serikali itatekeleza mpango wake kwa kuzingatia vipaumbele vinne vikuu vinavyolenga kuimarisha maendeleo ya vijana nchini.

Akizungumza leo bungeni mjini Dodoma wakati akiwasilisha mpango na makadirio ya matumizi ya Ofisi ya Rais – Maendeleo ya Vijana, Nanauka alisema lengo kubwa la vipaumbele hivyo ni kuwawezesha vijana kushiriki kikamilifu katika shughuli za kiuchumi, kijamii na kisiasa, pamoja na kuboresha ustawi wao kwa ujumla.

Kwa mujibu wa Nanauka, vipaumbele hivyo vitajikita katika maeneo yafuatayo:

Kwanza, kuimarisha ukuzaji wa biashara na uwezeshaji wa vijana kiuchumi, kwa lengo la kuwasaidia vijana wengi zaidi kujiajiri na kuajiriwa katika sekta za biashara na uzalishaji.

Pili, kuimarisha uratibu na ushirikishwaji wa vijana katika masuala ya kijamii, kiuchumi na kisiasa ili kuongeza ushiriki wao katika maendeleo ya taifa.

Tatu, kuimarisha uratibu wa elimu ya uraia, uzalendo pamoja na usimamizi wa shughuli za Mwenge wa Uhuru nchini.

Nne, kuimarisha ustawi na makuzi bora ya vijana ili kuhakikisha wanakua katika mazingira yanayowawezesha kufikia ndoto zao na kuchangia maendeleo ya taifa.

Nanauka alisisitiza kuwa mpango huo ni sehemu ya juhudi za serikali kuhakikisha vijana wanakuwa nguzo muhimu ya maendeleo ya taifa kupitia fursa za kiuchumi na ushiriki mpana katika ujenzi wa nchi.