Future Ashitakiwa na Ex Wake Kukwepa Majukumu ya Malezi ya Mtoto

Global Publishers
April 16, 2026
0 Comments

Rapa na mwimbaji maarufu wa Marekani  Rapa Nayvadius DeMun Wilburn ‘Future’ amejikuta tena kwenye mvutano wa kisheria na mama wa mtoto wake, Brittni Mealy, kuhusu malezi ya mwana wao wa miaka 13, Prince.

Kwa mujibu wa nyaraka za mahakama na barua iliyowasilishwa na Brittni, anadai kwamba Future hajamuona mwanawe kwa zaidi ya miezi 16 na hajakuwa na mawasiliano ya karibu naye katika kipindi hicho. Brittni anasema rapa huyo hajapiga simu, hajashiriki maendeleo ya shule, afya, wala shughuli za kila siku za mtoto wao.

Katika madai yake, Brittni anasisitiza kuwa hajawahi kumzuia Future kumfikia mtoto, akieleza kuwa baba huyo ana njia za moja kwa moja za mawasiliano, ikiwemo namba ya simu ya mtoto. Hata hivyo, anadai kuwa Future hajaitumia kwa ukamilifu kuwasiliana au kushiriki maisha ya mwanawe.

Pia anasema rapa huyo amekosa kuhudhuria matukio muhimu kama siku za kuzaliwa na mikutano ya shule, jambo analoliona kama kupoteza katika maisha ya mtoto wao. Brittni anadai pia kuwa Future alibadilisha namba yake ya simu na kuwahimiza watu walio karibu naye wasishirikiane na mtoto huyo, jambo ambalo limezidisha mvutano kati yao.

Katika upande wa kisheria, kuna pia mgogoro kuhusu madai ya Brittni kwamba Future alitakiwa kutekeleza amri ya mahakama ya kuweka bima ya maisha ya dola 500,000 (Tsh Bilioni 1.3) kwa ajili ya mtoto wao, kitu ambacho upande wa Future umekanusha, ukisema alishatekeleza wajibu huo.

Hata hivyo, hii ni kesi inayoendelea mahakamani, na pande zote mbili zimekuwa zikitoa madai yanayopingana kuhusu hali halisi ya uhusiano wa mzazi na mtoto.