Ndejembi awaita wabunge kutembelea maonyesho wiki ya nishati

Dodoma. Waziri wa Nishati, Deogratus Ndejembi amewahamasisha wabunge wa kutembelea maonyesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanayoendelea katika viwanja vya Bunge jijini Dodoma, yaliyoanza leo Jumatatu, Aprili 20-23, 2026.

Akizungumza leo Aprili 20,2026 wakati wa ziara yake kwenye mabanda ya maonyesho hayo, Ndejembi amesisitiza umuhimu wa wabunge kutumia fursa hiyo kukutana na wataalamu wa sekta ya nishati ili kupata uelewa mpana kuhusu utekelezaji wa miradi mbalimbali ya nishati inayoendelea nchini.

Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (Rea), Hassan Saidy akifafanua jambo katika Maonyesho ya Wiki ya Nishati yanayoendelea ndani ya viwanja vya Bunge Jijini Dodoma. Kushoto ni Waziri wa Nishati, Deogratius Ndejembi

Amesema maonyesho hayo yanalenga kuonesha mafanikio yaliyopatikana katika sekta ya nishati chini ya uongozi wa Rais Samia Suluhu Hassan.

Aidha, amesema maonyesho hayo yanabeba ubunifu na teknolojia mbalimbali za nishati safi ya kupikia, zikiwemo majiko ya umeme, majiko mbadala, majiko ya gesi ya kuchomea nyama, pamoja na jiko maalumu la umeme lililobuniwa kwa ajili ya watu wenye ulemavu wa macho.

Maonyesho hayo yanashirikisha taasisi mbalimbali zilizo chini ya Wizara ya Nishati, zikiwemo Shirika la Umeme Tanzania (Tanesco), Wakala wa Nishati Vijijini (Rea), Shirika la Maendeleo ya Petroli Tanzania (TPDC), Wakala wa Uagizaji wa Mafuta kwa Pamoja (PBPA), Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (Ewura) pamoja na Mamlaka ya Udhibiti wa Mkondo wa Juu wa Petroli (Pura).

Katika ziara hiyo, Waziri Ndejembi aliambatana na Katibu Mkuu wa Wizara ya Nishati (Umeme na Nishati Jadidifu), Felchesmi Mramba. Maonyesho ya Wiki ya Nishati 2026 yanatoa jukwaa muhimu kwa wabunge na wadau mbalimbali kujifunza, kuona ubunifu, na kubadilishana uzoefu kuhusu maendeleo ya sekta ya nishati nchini.