Netanyahu Akemea Mwanajeshi wa Israel Aliyeharibu Sanamu ya Yesu

Global Publishers
April 20, 2026
0 Comments

Waziri Mkuu wa Israel Benjamin Netanyahu amelaani vikali tukio lililosambaa mtandaoni likimuonesha mwanajeshi wa Israel akiharibu sanamu ya Yesu Kristo katika eneo la kusini mwa Lebanon.

Kwa mujibu wa taarifa yake, Netanyahu amesema ameshtushwa na kuhuzunishwa na tukio hilo, akisisitiza kuwa linaenda kinyume na maadili na misingi ya Israel kuhusu uhuru wa dini. Amesema tukio hilo halikubaliki na linachunguzwa na mamlaka za kijeshi ili kubaini kilichotokea na kuchukua hatua kali za kinidhamu dhidi ya mhusika.

Picha iliyosambaa mtandaoni inaonesha mwanajeshi huyo akitumia nyundo kuharibu sanamu ya Yesu Kristo, jambo lililosababisha hasira na mjadala mkubwa duniani, hasa miongoni mwa jamii za Kikristo.

Netanyahu amesema Israel inaheshimu uhuru wa kuabudu na kwamba ni moja ya nchi chache Mashariki ya Kati zinazolinda haki hiyo kwa watu wa dini zote. Ameongeza kuwa serikali inasikitishwa na tukio hilo na inalichukulia kwa uzito mkubwa.

Kwa upande wake, Balozi wa Marekani nchini Israel Mike Huckabee ametaka hatua za haraka, kali na za wazi zichukuliwe dhidi ya mhusika wa tukio hilo, akisisitiza umuhimu wa kuheshimu maeneo na alama za kidini.

Uchunguzi wa kijeshi unaendelea huku tukio hilo likizidi kuzua mijadala mikali mitandaoni na kimataifa kuhusu heshima ya dini na nidhamu ndani ya jeshi.