Global Publishers
April 20, 2026
0 Comments
Rais wa Marekani Donald Trump ameibua mjadala mkubwa wa kimataifa baada ya kutoa kauli kali akisema Marekani inaweza kuharibu kila kituo cha umeme na madaraja ndani ya Iran endapo hakuna makubaliano ya amani yatakayofikiwa ndani ya muda alioutaja.
Kupitia chapisho lake kwenye mtandao wa Truth Social, Trump alitumia maneno makali akisema “No more Mr Nice Guy” na kuongeza kuwa Iran lazima ikubali makubaliano la sivyo hatua kali za kijeshi zitachukuliwa. Pia alidai kuwa lengo lake ni kumaliza kile alichokiita machine ya mauaji ya Iran.
Kauli hiyo imekuja wakati mvutano ukiongezeka katika eneo la Ghuba, hasa baada ya taarifa za mashambulizi na mvutano katika njia muhimu ya usafirishaji mafuta ya Strait of Hormuz.

Kwa mujibu wa taarifa mbalimbali, Iran imeendelea kutoa vitisho vya kulifunga au kudhibiti zaidi eneo hilo endapo vizuizi dhidi yake havitaondolewa, huku pia ikishutumu Marekani kwa kuzuia meli zake.
Katika upande wa kidiplomasia, Marekani imetuma maafisa wake wakuu kwa mazungumzo ya amani, lakini bado hakuna makubaliano ya wazi yaliyofikiwa kati ya pande hizo mbili.
Wakati huo huo, vikosi vya Marekani vimeripotiwa kuwa katika hali ya tahadhari kubwa, vikijiandaa kuchukua hatua dhidi ya meli zinazohusishwa na Iran iwapo mgogoro utaendelea.
Hali hii imeongeza hofu ya uwezekano wa kuongezeka kwa mzozo katika eneo hilo muhimu la usafirishaji wa mafuta duniani, huku mataifa mbalimbali yakihimiza utulivu na suluhisho la kidiplomasia.