Mvutano wa kimataifa umeongezeka baada ya China kuonekana kupuuza hatua ya Marekani ya kuweka kizuizi katika Mlango wa Strait of Hormuz, huku meli yake iliyowekewa vikwazo ikipita karibu na vikosi vya majini vya Marekani bila kuzuiwa.
Kwa mujibu wa taarifa, meli ya China ijulikanayo kama Rich Starry, ambayo imekuwa chini ya vikwazo vya Marekani tangu mwaka 2023 kwa tuhuma za kushirikiana na Iran, ilisafiri katika eneo hilo huku ikipeperusha mzigo wa mapipa 250,000 ya methanol.
Hatua hiyo imekuja siku moja baada ya Donald Trump kuamuru Jeshi la Wanamaji la United States kuanza operesheni ya kuzuia usafiri wa meli kwenda na kutoka bandari za Iran, ikiwa ni sehemu ya mkakati wa kuishinikiza Tehran kukubali masharti mapya ya nyuklia.

Ingawa meli hiyo haikuingia moja kwa moja katika eneo lililozuiliwa, ilipita karibu na vikosi vya Marekani ambavyo vingekuwa na uwezo wa kuizuia, jambo lililotafsiriwa na wachambuzi kama ishara ya changamoto ya wazi dhidi ya hatua za Marekani.
Mvutano umeongezeka zaidi baada ya China kuonya kuwa hatua hiyo ya Marekani ni “hatari na isiyowajibika.” Msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje ya China, Guo Jiakun, alisema kuwa hatua hizo zinaweza kuongeza mivutano, kuhatarisha usalama wa usafiri wa majini na kudhoofisha juhudi za amani.

Wakati huo huo, soko la mafuta duniani limeathirika kutokana na hali hiyo, huku Iran ikitajwa kuchangia taharuki baada ya kuvuruga mtiririko wa biashara katika njia hiyo muhimu inayopitisha takribani asilimia 20 ya mafuta ya dunia.
Mvutano huo unatokana pia na mashambulizi yaliyofanywa na United States na Israel dhidi ya Iran mapema mwaka huu, hatua iliyosababisha majibu kutoka Tehran dhidi ya majirani zake wa Ghuba.
Makamu wa Rais wa Marekani, JD Vance, alisisitiza kuwa Marekani iko tayari kujibu hatua yoyote ya Iran, akitaja vitendo vya nchi hiyo kama ugaidi wa kiuchumi.
Kwa upande mwingine, washirika wa Marekani barani Ulaya wameanza kujitenga na operesheni hiyo. Waziri Mkuu wa Uingereza, Keir Starmer, amesema wazi kuwa nchi yake haitahusika katika mzozo huo, huku Rais wa Ufaransa, Emmanuel Macron, akisisitiza kuwa taifa lake litajikita katika kulinda uhuru wa usafiri wa majini badala ya kushiriki kwenye kizuizi hicho.
Hali hiyo imezua hofu ya kuongezeka kwa mvutano wa kijeshi kimataifa, huku wachambuzi wakionya kuwa hatua ndogo tu inaweza kuchochea mgogoro mkubwa zaidi wa kimataifa.