Simbu atetea nafasi ya pili Boston Marathon

Mwanariadha nyota wa Tanzania, Alphonce Simbu amepeperusha vyema bendera ya nchi baada ya kumaliza katika nafasi ya pili kwenye Mbio za Boston Marathon ambazo zimefanyika leo huko Boston Marekani.

Simbu ameshika nafasi hiyo akitumia muda wa saa 2:02:47 huku kinara akiwa ni John Korir wa Kenya aliyetumia muda wa saa 2:01:52.

Katika mbio za leo, aliyeshika nafasi ya tatu upande wa wanaume ni Benson Kipruto kutoka Kenya ambaye ametumia muda wa saa 2:02:50 akizidiwa kwa sekunde tatu tu na Simbu.

Hii ni mara ya pili mfululizo kwa Simbu kumaliza katika nafasi hiyo kwani hata mwaka jana aliondoka na medali ya shaba.

Korir aliyeibuka mshindi ameondoka na kitita cha Dola 150,000 (Sh389 milioni), Simbu amevuna Dola 75,000 (Sh195 milioni) na Kipruto aliyemaliza akiwa mshindi wa tatu ataondoka na Dola 40,000 (Sh104 milioni).

Boston Marathon ni miongoni mwa mashindano makubwa saba ya riadha duniani kutokana na thamani, zawadi kwa washindi na mvuto wake kwa wapenzi wa riadha duniani.