Nane zafuzu robo fainali Kombe la FA Unguja

TIMU nane zimetinga hatua ya robo fainali ya Kombe la FA Kanda ya Unguja, zikiwemo klabu mbili kutoka Ligi Daraja la Kwanza ambazo ni Raskazone na Black Sailor, huku sita zikitoka Ligi Kuu Zanzibar ambazo ni KVZ, Mlandege, JKU, KMKM, Kipanga na Mafunzo.

KVZ imekamilisha ratiba hiyo baada ya kuifunga Zimamoto mabao 3-1, wakati Kipanga ikiibuka na ushindi wa mabao 2-1 dhidi ya Malindi, Aprili 16, 2026 kwenye Uwanja wa Mao Zedong, Unguja.

Kocha Msaidizi wa KVZ, Ali Khalid ‘Kisoda’, amesema siri ya ushindi huo ni nidhamu ya wachezaji kufuata maelekezo ya benchi la ufundi pamoja na kujituma uwanjani.

“Mkakati wa KVZ ni kupata ubingwa kwa kila kombe inayoshiriki, hivyo ushindi huu ni njia ya kuufikia ubingwa,” amesema kocha huyo.

Kwa upande wa Zimamoto, Kocha Mkuu Hassan Abdulrahman alikiri kuzidiwa eneo la kiungo kuwa sababu kuu ya kupoteza mechi hiyo.

Wachezaji wa eneo la kati hawakutimiza majukumu yao ipasavyo, hivyo hilo limekuwa faida kwa wapinzani wetu kutengeneza nafasi na kushinda,” amesema.

Aliongeza timu yake itarejea mazoezini ili kurekebisha makosa kuelekea mechi zijazo za Ligi Kuu Zanzibar.

Hatua ya robo fainali ya mashindano hayo inatarajiwa kuchezwa kuanzia Mei 5 hadi 8, 2026, kwenye Uwanja wa Mao.